MWENDO UMEGOTA UKINGONI, WAKATI WA KUJIPANGA UPYA - Dizo Click

Dizo Click

Hot

Post Top Ad

Tuesday, 6 September 2022

MWENDO UMEGOTA UKINGONI, WAKATI WA KUJIPANGA UPYA

 


MWENDO ambao tulianza nao kwa wachezaji wa Timu ya  Taifa Stars katika kuwania kufuzu Kombe la Mataifa Afrika, (CHAN) dhidi ya Uganda huohuo tumemaliza nao somo kubwa kwetu.

Kwenye mchezo wa kwanza uliochezwa Uwanja wa Mkapa tuliona kwamba tulipoteza kwa kufungwa bao 1-0 na uweza kujipa matumaini kwamba tunakwenda kupata matokeo ugenini.

Ilikuwa ni maumivu kwa mara nyingine tena baada ya mchezo wa pili pia kuisha kama ule wa awali kwa kupoteza mchezo tena.

Mabao 3-0 ambayo tumefungwa yamezima matumini ya Stars kuweza kusonga mbele na sasa wamerejea kuweza kuanza mpago kazi upya kwa wakati ujao.

Tuliongea hapa kwamba sio kazi nyepesi kuweza kuwakabili Uganda ambao nao walikuwa wanahitaji nafasi ya kuweza kusonga mbele.

Haijawezekana tumekwama na kutolewa kwa jumla ya mabao 4-0 hili ni la maumivu kwa kila Mtanzania na muhimu kwa wachezaji kujiuliza kwa wakati mwingine pale watakapoitwa kufanya kweli.

Mechi mbili bila kupata bao hii inatoa taswira kwamba taifa linasumbuliwa na tatizo la ushambuliaji na kufungwa mabao pia inamaanisha bado kwenye safu ya ulinzi kuna tatizo.

Hapo ndipo ambapo kazi inabidi ianze kufanyika kwa vitendo kuanza kutengeneza vipaji vipya na kuvikuza vile ambavyo vipo kwa ajili ya kuwatumia kwa wakati ujao.

Watanzania furaha yao ipo kwenye ushindi basi ni muda   wa kuwekeza kwa vitendo kwenye kuibua, kukuza, kuvilinda na kuvitumia vipaji ambavyo vitaibuliwa sio kwa ajili ya leo bali kesho.

Ikiwa maandalizi yataanza kwa wakati huu kuendeleza vile ambavyo tunavyo itatupa matokeo mazuri kesho kwa kuwa mpango kazi wetu utafanya kazi nzuri na matokeo yataonekana.

Wachezaji wamekuwa wakijituma kutafuta matokeo ila wakati mwingine wanashindwa kuyapata kutokana na kukutana na wapinzani ambao ni imara zaidi yao.

Makosa ya mara kwa mara kwenye safu ya ulinzi na ushambuliaji yanawapa nafasi wapinzani kujua namna ya kuwakabili Stars kwenye mechi ambazo wanacheza nao.

Kwa sasa sio muda wa kuendelea kulaumu bali kuja na mpango kazi ambao utatupa matokeo chanya baada ya miaka mitatu ijayo ama mitano.

Kuandaa timu bora hakuwezi kuleta majibu kwa muda mfupi wa mwezi mmoja ama miwili lazima kuwe na mpango kazi wa miaka mitatu mpaka mitano ambayo itawafanya wachezaji hao wawe ni kizazi kimoja.

Vipaji Tanzania vipo, uwezo wa wachezaji kupata matokeo kwenye mechi zao nyumbani na ugenini upo lakini lazima wapewe maandalizi mazuri na mbinu ambazo zitawafanya wafanye kazi kwa kujituma muda wote.

Kwa wachezaji ambao wataitwa kwenye mashindano mengine ndani ya timu ya Taifa ya Tanzania jukumu lao liwe moja kujitoa bila kuogopa na kutengeneza nafasi zaidi kushinda.

Ni mara chache kwa nafasi kupatikana hasa uwanjani na ikipatikana kujirudia pia inakuwa ni ngumu hivyo ni muhimu kuweza kutumia nafasi kwa umakini na kupata matokeo mapema.

Kwa mechi za nyumbani itakuwa somo kwa namna ambavyo Uganda wao walikuwa wakifanya, muda wote wanacheza na kuleta presha kwa wapinzani.

Kwa hilo tuna amini wakati ujao kutakuwa na mabadiliko kwa wachezaji katika kutumia uwanja wa nyumbani na ule wa ugenini.

Kazi bado ipo na ni muhimu kuwa na mpango kazi imara utakaotupa matokeo na kuwapa furaha mashabiki na Watanzania kiujumla.

 

 

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad