JESHI la Polisi Kanda Maalumu ya
Dar Es Salaam limepiga marufuku disko toto kipindi cha sikukuu ya Maulidi na
kuwataka wazazi kuwa karibu na watoto wao kipindi hicho ili kuhakikisha usalama
wao.
Akizungumza
Dar es Salaam, Kamishna wa kanda hiyo Simon
Sirro alisema jeshi hilo kwa kushirikiana na vyombo vingine vya ulinzi na
usalama wamejipanga kuhakikisha siku hiyo inakuwa ya utulivu zaidi.
![]() |
| Kamishna wa Kanda Maalum ya Dar Es Salaam Simon Sirro |
“Tumejipanga na kutakuwa na
makachero kila kona, doria za miguu, askari kanzu, askari wa mbwa na farasi, jeshi
la kuzuia fujo (FFU) na magari ya doria ili kuhakikisha amani na usalama
unatawala kila mahali,” alisema Sirro.
Kamishna Sirro aliwataka wazazi
na walezi kuwafunza watoto wao maadili mema ili kujiepusha kuwa katika makundi
mabaya kama Panya road, ulevi na vurugu kwa kipindi hicho,
“Wazazi tuwalinde watoto wasizurule ovyo pia
tukielekea maeneo ya starehe nyumbani tuache ulinzi wa uhakika,” alisema.
Katika hatua jeshi hilo
limefanikiwa kuwakamata watuhumiwa sugu 103 wa makosa mbalimbali jijini Dar es
Salaam kwa kipindi cha kuanzia Desemba 2 hadi 8 mwaka huu.
Makosa hayo ni pamoja na kucheza
kamari, wizi wa magari, kutengeneza kunywa na kuuza pombe haramu ya Gongo, na
kueleza kuwa oparesheni hiyo itakuwa endelevu.
Pia jeshi hilo kupitia kikosi
cha usalama barabarani kanda maalum ya Dar es Salaam wamefanikiwa kukusanya
zaidi ya sh. Milioni 400 kupitia tuzo za makosa ya kiusalama barabarani,
Kiasi hicho kimepatika kwa
kipindi cha kuanzia Desemba 2 hadi 7 mwaka huu ambapo jumla ya makosa 15,053
yalikamatwa.

No comments:
Post a Comment