Simba waipokea Yanga Bandari
Waandishi Wetu
MASHABIKI wa Simba jana walijitokeza kwa wingi Bandari ya Dar es Salaam kuwapokea watani zao wa jadi Yanga ambao waliwasili wakitokea Zanzibar.
Yanga iliondoshwa katika hatua ya nusu fainali ya Kombe la Mapinduzi baada ya kupoteza kwa kufungwa penalti 9-8 mbele ya Azam FC katika mchezo wa nusu fainali ya kwanza.
Majira ya saa saba tayari katika Bandari hiyo kulikuwa na mashabiki wengi wa Simba ambao walikuwa wamevaa jezi zenye nembo ya Simba huku wakishangilia kwa mtindo wa Fiston Mayele pale akifunga pamoja na Pape Sakho akifunga.
Baada ya wachezaji kuwasili Bandarini mashabiki hao wa Simba walisikika wakiimba :"Tunalitaka kombe letu,tunalitaka kombe letu,".
Pia walipata muda wa kupiga picha na Mayele ambaye ni kinara wa utupiaji ndani ya Yanga kwenye ligi akiwa na mabao matano na pasi moja.
Hassan Bumbuli, Mkuu wa kitengo cha Habari Yanga amesema kuwa hesabu zao kwa sasa ni kwenye ligi kwa kuwa bado wana kazi ya kufanya.
"Bado tuna kazi ya kufanya hasa baada ya kushindwa kutwaa taji la Mapinduzi na ilikuwa ni malengo yetu kilichotokea ni matokeo, " alisema.
No comments:
Post a Comment